Iglesia Catolica Palmariana

KANISA MOJA, TAKATIFU, KATOLIKI LA MITUME LA PALMAR

Kanisa Katoliki la Kweli la nyakati zote,
lililoanzishwa na Bwana Wetu Yesu Kristo.
Urithi Halali wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro,
Chini ya utawala wake Papa Mkuu Petro III,
De Glória Ecclésiæ

Kanisa Katoliki la Kweli la nyakati zote, lililoanzishwa na Bwana Wetu Yesu Kristo. Urithi Halali wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Chini ya utawala wake Papa Mkuu Petro III,
De Glória Ecclésiæ

Hii ni tovuti rasmi ya Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar, iliyoidhinishwa na Baba Jenerali wa Jamii ya Wakarmeli wa Uso Mtakatifu, Baba Mtakatifu Petro wa tatu. Kwa uchunguzi wowote zaidi kuhusu Kanisa Katoliki la Palmar, ni muhimu kuenda kwenye akaunti za kijamii zilizoidhinishwa na Kanisa Katoliki la Palmar pekee, ambazo, baadhi zimeandikwa chini ya ukurasa huu. Machapisho mengi kwenye mitandao hayana ukweli wowote, ni ya kutatanisha na yasiyo sahihi.

Lipo Wapi Kanisa Katoliki La Nyakati Zote?

Historia Fupi

Mnamo tarehe thelathini (30) Machi mwaka wa 1968, Mama Bikira Maria wa Karmeli alionekana kwa mara ya kwanza na wasichana wanne, kutoka kijiji cha El Palmar de Troya, Seville, Uhispania, juu ya mti wa lentiski. Hakuna kitu chochote kilichosalia katika mti wa tokeo hili la kwanza kwani watu walikata matawi yake kama masalio ya thamani. Papo hapo, msalaba mdogo wa mbao uliwekwa na kando yake maombi yalisemwa na wajumbe wakapokea ziara kutoka Mbinguni. Kwa njia hii, mahali palipochaguliwa na Mama Bikira Maria alipotokea kwa mara ya kwanza, paliwekwa ukumbusho. Baadaye, Picha za Uso Mtakatifu wa Yesu na Mama Yetu wa Palmar Aliyetawazwa, ziliwekwa hapo.

Kufuatia wale wasichana wanne wa kwanza, kulikuwa na wajumbe wengine ambao walikuwa na furaha ya ajabu na walipokea jumbe muhimu kutoka mbinguni.

Mahali hapa Patakatifu, ambapo katika siku zijazo pangekuwa Kiti cha Kanisa Takatifu la Palmar, palikuwa pametayarishwa na Mama Bikira Maria kwa zaidi ya karne moja kwa kutokea kwake katika sehemu tofauti tofauti kama vile: La Salette mnamo mwaka wa 1846, Lourdes mnamo mwaka wa 1858, Fatima mwaka wa 1917, Garabandal mwaka wa 1961, na maeneo mengine mengi.

Ni mahali Patakatifu pa Lentisko ya El Palmar de Troya, ambapo hali ya wasiwasi katika Kanisa Katoliki ilifunuliwa hatua kwa hatua, matukio yatakayopata kanisa katika siku zijazo, adhabu na maafa yatakayotokea kwa wanadamu wote ambayo, yote yangeweza kupunguzwa tu, kwa sala, kwa toba na kwa kukomesha maendeleo yenye madhara sana yaliyoletwa ndani ya kanisa, kwa mfano: watu kupokea Hostia Takatifu mkononi, kuipokea wakiwa wamesimama badala ya kupiga magoti, mapadre na watawa wengi kuweka kando desturi zao takatifu…

Uharibifu wa Kanisa kwa njia ya kubatili mafundisho asili ya kanisa, mabadiliko ya liturujia, kukomeshwa kwa Sadaka Takatifu ya Misa na kuondolewa kwa Bikira Maria Mtakatifu na Watakatifu wengi kutoka kwa makanisa, ulisababisha uharibifu wa kiroho kwa idadi kubwa ya washiriki wa kanisa.

Mama Bikira Maria, kama Mama wa Kanisa, baada ya maonyo mengi, alionekana katika kijiji hiki ambapo, kama Mchungaji na Mwalimu Mtakatifu, hatimaye alijiweka tayari kulifanya upya kanisa, kutokana na kwamba Kanisa la Roma lilikuwa kwenye njia ya uasi. Kuanzia wakati huo, kuliendelea kuwa na matukio yasiyohesabika ya Mama Bikira Maria na ya Bwana Wetu Yesu Kristo, ya Mungu Baba, na ya idadi kubwa ya Watakatifu, ambao walitayarisha hatua kwa hatua matukio yajayo katika Kanisa Takatifu.

Jumbe za mara kwa mara zilizopokelewa na wajumbe wengi, miujiza ya umma, uponyaji na matukio mengine ya mafumbo huko El Palmar, zilivutia mtiririko wa mahujaji, sio tu kutoka Uhispania, bali pia kutoka sehemu zote za ulimwengu, wakitafuta ukweli asili, usiopatikana tena kwa Kanisa la Roma.

Mjumbe mkuu aliyechaguliwa na Mungu kueneza kila mahali jumbe ambazo zilipaswa kutolewa huko El Palmar, alikuwa kijana kutoka Seville, aliyezaliwa tarehe 23 Aprili, mwaka wa 1946, ambaye angekuja kuwa Papa Mkuu wa siku zijazo wa Kanisa Takatifu na makao yake yakiwa katika mahali hapa Patakatifu: Gregory XVII (jina la kuzaliwa likiwa Clemente Domínguez y Gómez). Kama mjumbe mkuu wa El Palmar, hakuwa tu mpokeaji muhimu wa ujumbe; Badala yake, Mama Bikira Maria aliongoza maombi yake pamoja na matukio mengi ya mafumbo aliyomkabithi, ishara dhahiri ambazo zilithibitisha ukweli wa maneno hayo: furaha za ajabu, wongofu, uponyaji wa kimiujiza, utokeaji wa madonda matakatifu, na kadhalika. Madonda matakatifu aliyopata yalikuwa ishara wazi kabisa kwa yeyote ambaye kwa unyenyekevu alitaka kuukubali ukweli. Kuanzia wakati huo, Clemente Domínguez alikuwa atimize moja ya misheni ngumu sana ambayo mtu yeyote anaweza kuwa nayo; hata hivyo, kwa msaada na nguvu za Mungu na Mama Bikira Maria, alivumulia na kupigana kwa bidii na ushujaa katika kuutetea ukweli.

Clemente alienda safari nyingi sana, akihubiri kuhusu El Palmar, akialika ulimwengu kupata kujua sehemu moja  ya wokovu katika nyakati hizi za uharibifu, mkanganyiko na giza linalotawala katika Kanisa la Roma. Licha ya mashambulizi, ukosoaji na kashfa zilizoanzishwa dhidi yake, alikuwa mwaminifu kwa misheni aliyokabidhiwa na alijitolea kwa ushujaa na nguvu kwa kazi hiyo ngumu ya kueneza maneno aliyopokea kutoka mbinguni.

Uendelezaji wa sala na toba ya kudumu, kama Yesu na Mama Bikira Maria walivyoagizia katika Mahali hapa Patakatifu, na ambayo wafuasi wake walifanya kwa bidii, haukuchukua muda mrefu kuzaa matunda.

Miaka michache baada ya tokeo hilo la kwanza, msingi wa kiroho ulipangwa katika utaratibu muhimu zaidi wa Kidini wa Nyakati za mwisho. Kuteuliwa na kuwekwa wakfu kwa viongozi wapya wa kanisa katika matawi yake tofauti ilitengeneza Chuo cha Maaskofu na Kitume ambacho, kilikuwa na idadi kubwa ya washiriki ili kusaidia kulinda desturi takatifu za kikatoliki katika Mahali hapa Patakatifu. Mahali hapa palichaguliwa na Mungu kuhifadhi usafi na nguvu za ukatoliki na hivyo kuwa makao ya Baba Mtakatifu kwa wakati ujao. Wapalmar walijitayarisha sio tu kiroho bali pia walianza kujenga hekalu la Mungu ambapo ibada ya kweli ingefanywa daima, iliyoharibika zaidi kote ulimwenguni.

Kwa hivyo, katika Mahali hapa Patakatifu ambapo Bikira Maria alionekana katika tokeo la kwanza, kwa ombi lake kama Mama Mzazi, kanisa kuu la ‘Mama Yetu Maria Mwenye Taji’, lilijengwa. Jitihada zilizofanywa na wapalmar wa kwanza zilikuwa kubwa ili ndoto hii ipate kuwa ya kweli, kwa imani na maombi yao ya uaminifu yalijibiwa na Mwenyezi Mungu.

Wakati wa kifo cha Baba Mtakatifu Paulo VI mwaka wa 1978, mjumbe mkuu Clemente, ambaye wakati huo alikuwa Askofu, alichaguliwa na kutawazwa na Yesu kuwa Baba Mtakatifu katika maono ya kustaajabisha huko Santa Fe de Bogota, Colombia. Baba huyu Mtukufu Gregori wa kumi na saba aliitisha mabaraza makuu mawili matakatifu yaliyohusika na ufafanuzi wa kanuni za Imani, ambayo yalileta mwanga wa vito vya ukweli kutoka kwa hazina takatifu ya ufunuo wa kimungu, kwa mfano maandishi tofauti kuhusu mafundisho na maadili.

Baba Mtakatifu wa kweli kwa sasa anaishi El Palmar de Troya, akitawala kwa jina la Petro III. Yeye ndiye Papa Halisi, Kasisi wa Kristo. Yeyote asiye naye, hayuko pamoja na Kristo. Ni Mapadre wa Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar pekee, ndio wenye uwezo halisi wa kusimamia Sakramenti Takatifu na kuadhimisha Sadaka Takatifu ya Misa.

Kwa sasa, waumini wengi kutoka mataifa mbalimbali hukusanyika kwa hija katika Mahali hapa Patakatifu, kutoa Ibada Takatifu kwa Mungu na heshima kwa Mama Bikira Maria, na kufanya malipizi kwa ajili ya dhambi za wanadamu. Ibada ya hapa yenye ucha Mungu na adhimu na maandamano ya kiroho, yanaimarisha Imani, huku tukisubiri ushindi wa Kanisa Takatifu la Palmar.

Alama za Kanisa la Kweli

1. Kanisa la Kristo ni: Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar.

  • Ni Moja katika imani, kwasababu ukweli uliofunuliwa na Mungu ni sawa kwa wote, Moja katika utawala, kwasababu kuna kiongozi mmoja mkuu anayeonekana, Baba Mtakatifu, na pia Moja katika Sakramenti, kwasababu ziko sawa kwa waumini wote wa Kanisa.
  • Ni Takatifu, kwasababu Mwanzalishi wake ni mtakatifu, mafundisho yake ni matakatifu, lengo lake na waumini wake ni kuazimia kuwa watakatifu.
  • Ni Katoliki, kwasababu lipo ulimwenguni kote, linakubali ukweli wote na ni la watu wote.
  • La Mitume, kwasababu uongozi wake na mafundisho yake yanatokana na Mitume.
  • La Palmar, kwasababu makao yake makuu sasa yako El Palmar de Troya (Seville, Uhispania).

2. Kanisa la kweli la Kristo halina dosari, halishindwi na haliharibiki. Mwanzilishi wake Mtukufu (Yesu) aliahidi : “Milango ya kuzimu haitalishinda”.

3. Kanisa la kweli la Kristo pia linaitwa ‘Kanisa la Kikristo la Palmar la Wakarmeli wa Uso Mtakatifu’ au ‘Kanisa la Palmar’, kwasababu kimsingi, ni sawa na kusema ‘ Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki, la Mitume la Palmar.

4. Kanisa la Palmar ndilo Kanisa la pekee na la kweli la Kikristo, jina ambalo lilipewa na Kristo, Mwanzilishi wake.

5. Tarehe 6 Agosti, 1978, baada ya kifo cha Baba Mtakatifu Paulo VI, Bwana wetu Yesu Kristo, akifuatana na Mitume watakatifu, Petro na Paulo, alimchagua na kumtawaza upya, Mtakatifu mkubwa, Gregory XVII. Tangu wakati huo, kanisa la Roma lilikoma kuwa kanisa la kweli.

6. Kwa ajili ya uasi wa kanisa la Roma, Kristo alihamisha makao yake makuu ya Kanisa kutoka Roma hadi El Palmar de Troya, mnamo tarehe 9 Agosti, 1978. Kwa kuchaguliwa kwa Baba Mtakatifu Gregory XVII na uhamisho wa makao makuu, Kanisa la kweli la Kristo lilipokea jina la Palmarian.

7. Roho Mtakatifu, ni Roho ya Kanisa moja la kweli, yaani, Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar. Roho Mtakatifu hawezi kukaa kwa roho za walio nje ya Kanisa Takatifu.

8. Jamii ya Kanisa la Palmar la Wakarmeli wa Uso Mtakatifu kwa muungano na Yesu na Maria, kwa ujumla, ina matawi matatu: Mapadre, Watawa na Waumini wa kawaida.

9. Tarehe 30 Julai, 1982, Baba Mtakatifu Gregory XVII aliondoa mamlaka yote kutoka kwa Maaskofu, Makasisi na Mashemasi walio nje ya Kanisa la kweli, Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar. Vile vile, aliondoa utakatifu wa masalio yote; sanamu, vitu vilivyotumiwa katika ibada, madhabahu na kadhalilka ya makanisa yaliyoasi, yenye uzushi na mafarakano. Zaidi ya hayo,uwepo wa Ekaristia Takatifu ya Kristo na Maria ulitoweka katika hema zote takatifu za ulimwengu zisizo chini ya Kanisa la Palmar.

10. Maaskofu, Mapadre na Mashemasi nje ya Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume la Palmar hawana uwezo halali wa kufanya huduma yoyote ya kikuhani au kipadre.